KANISA KATOLIKI LAANDAA WAUMINI UCHAGUZI 2010

KANISA Katoliki nchini limeanzisha programu maalumu yenye lengo la kuwafundisha waumini wake namna ya kupata viongozi bora katika uchaguzi mkuu ujao mwakani. Mbali na hilo, kanisa hilo limeonya baadhi ya wanasiasa ambao wamekuwa wakipinga viongozi wa dini kuingilia masuala ya siasa na kueleza kuwa kamwe vitu hivyo haviwezi kutenganishwa.

Kanisa hilo limesema Serikali imepoteza imani yake kwa wananchi kutokana na kuendelea kukumbatia mafisadi kwa kushindwa kufikia maamuzi ya haraka ya kesi za tuhuma za ufisadi, jambo ambalo kanisa hio limesema litazidi kukemea bila woga. Akizungumza katika maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu ya Kutoa Komuniyo ya Kwanza kwa vijana wa Parokia ya Manzese, Jimbo Kuu la Dar es Salaam, Padri Baptiste Mapunda wa Shirika la Wamisionari wa Africa, alisema wakati umefika chama tawala CCM kukubali kubalika kwani Watanzania sasa wameelimika na hawako tayari kuendelea kuburutwa.

"Maovu ni mengi sana katika nchi hii na yanasababisha kuporomoka kwa maadili, ambapo vyombo vya habari vinafanya kazi kubwa kuyagundua na kuhabarisha umma na sasa wananchi wameshaamka na wanataka demokrasia ya kweli hivyo utawala lazima ubadilike," alisema Padri Mapunda. Akifafanua kuhusu uchaguzi mkuu ujao mwakani, Padri Mapunda alisema viongozi wa kanisa hilo wamekubaliana umuhimu wa kufundisha waumini wao na tayari wameanza kutoa mafunzo na semina mbalimbali kuwaelimisha namna ya kupata viongozi bora na kwamba viongozi hao watapatikana kutokana na uwezo wao si kwa kutoa rushwa.

"Viongozi wasio na uwezo ndio wanaotumia nguvu kubwa (rushwa) kupata nafasi za kuingia madarakani ambapo badala ya kulitumikia Taifa wanafikiria kujilimbikizia mali ili kufidia gharama walizotumia wakati wa uchaguzi, hivyo tuwe makini nao,"alisisitiza Padri Mapunda. Alisema wakati wa mabadiliko ukifika hauepukiki hivyo kama viongozi hawako tayari kubadilika mabadiliko yatawabadilisha kwa lazima kwani huo ndiyo mfumo wa maisha ya binadamu.

Alisema suala la ufisadi limekuwa wimbo usio na mwitikio kwa wananchi kutokana na Serikali kuchukua muda mrefu kumaliza kesi za ufisadi jambo ambalo linaweza kupatiwa ufumbuzi mapema. Alisema maovu yanayoendelea kutokea hapa nchini kama yale ya ufisadi na mengine yanatokana na ubinafsi, mmomonyoko wa maadili na matumizi mabaya ya madaraka miongoni mwa watu wachache wenye nafasi za juu Serikalini.

"Tatizo ni ubinafsi wa watu wachache wenye tamaa ya kujilimbikizia mali ndio unaoumiza Watanzania wengi," alisema na kuongeza kuwa ni "Nguvu za Mungu pekee ndizo zitakazosaidia kupiga vita ufisadi huu unaoshamiri kwa kasi" Alisema neno, 'ufisadi' na 'rushwa' sasa yamekithiri katika vinywa vya Watanzania na kuonya kuwa hali hiyo inaonesha kuwa sasa wamechoka na wakiamua kupambana na uovu huo wataweza.

Alisema ipo haja ya kufanyika mabadiliko Katiba kwa ya sasa imejaa viraka na haitoshelezi mahitaji ya demokrasia ya kweli.Alieleza kuwa hali hiyo inayotoa nafasi kwa watu kufanya maovu wanavyotaka bila ya kuchukuliwa hatua stahiki. Alisema kuwa Katiba hiyo ni ya muda mrefu na ina maelekezo yaliyopitwa na wakati hivyo haikidhi mahitaji ya ulimwengu wa sayansi na teknolojia na inachangia kukwamisha maendeleo ya Taifa.

''Tunahitaji mapinduzi ya kikatiba wakati tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu kwani hata mtu asiye msomi anaweza kugundua udhaifu wa Katiba yetu na kama viongozi hawatakuwa tayari nguvu ya watu italeta mabadiliko,"alisema. Padri Mapunda aliongeza kuwa Serikali ya Tanzania imeshindwa kuonesha demokrasia ya kweli kwa kushindwa kuwa na Tume Huru ya Uchaguzi jambo ambalo linasababisha vyama vya siasa kulalamika kila uchaguzi unapofanyika kwa kutotendewa haki.

Alisema NEC inateuliwa na viongozi wa chama tawala na wakati huo huo inasimamia uchaguzi wa viongozi wa vyama vyote ambapo mwanya wa kupendelea CCM unakuwa mkubwa. "Hakutakuwa na amani hadi mabadiliko haya yafanyike kama jipu litaendelea kupakwa mafuta ipo siku litapasuka tu, hivyo ni bora marekebisho yakafanyika mapema kuliko kusubiri misukumo kutoka kwa wananchi waliochoshwa na Katiba hiyo," alisema.

Amevitaka vyama vya siasa kuacha ubinafsi kwani ni vigumu kwa chama kimoja kuchukua nchi kwa sasa ikiwa havina ushirikiano na badala yake vinapaswa kuweka malengo ya muda mrefu kwa kuzingatia maeneo ambayo vinaweza kuunganisha nguvu na kuweka mgombea anayekubalika na wengi. Alisema kuwa malumbano baina ya vyama vya upinzani yamezidi kushamiri kutokana na mamluki walio ndani ya vyama hivyo kukwamisha mikakati endelevu na kushindwa kufikia malengo na kupoteza imani kwa wananchi hata pale wanapokuwa na malengo mazuri. "Malumbano hayo yameikumba hadi CCM kufikia kiasi cha kupigana wakigombe madaraka hali ambayo inadhihirisha kuwa utawala sasa unahitaji mabadiliko kwani baadhi ya viongozi wamekosa uadilifu,'' alisema Padri Mapunda.

Please Select Embedded Mode To Show The Comment System.*

Postagem Anterior Próxima Postagem